Tuesday 22 April 2014

LW 109: COMMUNICATION SKILLS FOR LAWYERS --------- BY. MWL. JAPHET MASATU

What Skills and Aptitudes Does This Lawyer Need?


Answer

A lawyer should possess; intellectual skills, analytical skills, socials skills and communication skills. These skills enable them to create logical arguments, interact well with their clients and communicate well when they presenting their arguments before the jury either in writing or orally.

TANZU NA VIPERA VYA FASIHI SIMULIZI

TANZU    NA   VIPERA   VYA    FASIHI   SIMULIZI.

Vigezo alivyovitumia Mulokozi katika kugawa tanzu na vipera vya Fasihi Simulizi katika Jarida la Mulika (1989) namba 21.
 (Kikosi Kazi)
Kwa mujibu wa Mulokozi katika Mulika namba 21(1989). Pamoja na kwamba Fasihi ni kongwe lakini kitaaluma bado ni changa kwa sababu ilianza kuchungunzwa hivi karibuni. Hivyo imepelekea kutokuwepo kwa nadharia, marejeo, wala istilahi zenye kutosheleza mahitaji ya taaluma hiyo. Tatizo hili linadhihirika pale tunapoangalia kazi za wataalamu mbalimbali kuhusu tanzu za Fasihi Simulizi. Kwa upande wa nadharia kitabu pekee kinachozijadili tanzu za Fasihi Simulizi kwa urefu ni kitabu cha Ruth Fennegan kinachoitwa Oral Literature in Africa (1970). Kwa upande wa Kiswahili hakuna kitabu kinachojadili uwanja wa tanzu za Fasihi Simulizi. Badala yake kunamiongozo michache kwa ajili ya shule za sekondari kama vile Balisidya, N (1975) na Taasisi ya Elimu (1987)
Mulika namba 21 ni jarida la kitaaluma linalotoa fursa kwa wataalamu, waalimu na wanafunzi katika kujadili mada mbalimbali za kiswahili. Jarida hili lililoandikwa mwaka 1989 ndani yake kuna makala ya Fasihi Simulizi inayohusu tanzu za Fasihi Simulizi na vipera vyake iliyoandikwa na M.M.Mulokozi.

Hivyo basi kutokana na kukosekana kwa nadharia zinazoongoza ugawaji wa tanzu za Fasihi Simulizi ya Kiswahili wataalamu wengi wamekuwa wakitumia vigezo mbalimbali ambavyo ni maudhui, fani, matukio, idadi ya waimbaji, vifaa vinavyotumika na namna ya uimbaji.
Fasihisi Simulizi imejadiliwa na wataalamu mbalimbali miongoni mwa waalamu hao ni M.M.Mulokozi (1996) anasema Fasihi Simulizi ni fasihi inayotungwa au kubuniwa kichwani na kuwasilishwa kwa hadhira kwa njia ya mdomo na vitendo bila kutumia maandishi.
TUKI (2004) Fasihi Simulizi ni kazi ya fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo kama vile; hadithi, ngoma na vitendawili. 
Hivyo basi Fasihi Simulizi ni fasihi inayotokana na maneno ambayo huzungumzwa, hutolewa au kuimbwa ambapo mtungaji na mwasilishaji hutumia sanaa.
Tanzu ni istilahi inayotumiwa kuelezea au kurejelea aina ya kazi mbalimbali za kifasihi. Inawezekana utanzu mkuu kuwa na vitanzu vingine mbalimbali kwa mfano, tanzu kuu za kifasihi ni Riwaya, Tamthilia, Shahiri, Novela, Insha na Hadithi (Wamitila (2003).
Vipera ni dhana inayotumiwa kuelezea vijitanzu katika fasihi hasa fasihi simulizi. Mfano: semi methali, mafumbo, vitendawili nakadhalika. (Wamitila 2003)
M.M.Mulokozi katika makala yake ya tanzu za Fasihi Simulizi iliyo katika jarida la Muulika namba 21(1989) amezigawa tanzu na vipera vya Fasihi Simulizi kwa kutumia vigezo viwili ambavyo ni,kigezo cha kwanza ni umbile na tabia ya kazi inayohusika na kigezo cha pili ni muktadha na namna ya uwasilishaji wake kwa hadhira.
Umbile na tabia ya kazi inayohusika: katika kigezo hiki Mulokozi ameangalia vipengele vya ndani vinavyoiumba sanaa hiyo na kuipa muelekeo au mwenendo. Baadhi ya vipengele hivyo vya ndani ni namna lugha inavyotumika (kishahiri, kinathari, kimafumbo, kiwimbo na kighani), muundo wa fani hiyo na wahusika.
Kwa upande wa muktadha na namna ya uwasilishaji amezingatia kuwa, Fasihi Simulizi ni tukio hivyo huambatana na muingiliano wa mambo matatu ambayo ni muktadha, watu na mahali. Mwingiliano huu ndio unaotupa muktadha na muktadha ndio unaoamua fani fulani ya Fasihi Simulizi ichukue umbo lipi, iwasilishwe vipi kwa hadhira, kwenye wakati na mahali hapo. Hivyo hadithi inaweza kugeuzwa wimbo, utendi unaweza kuwa hadithi na wimbo unaweza kugeuzwa ghani au usemi kutegemea muktadha unaohusika (Mulokozi 1989).
Kwa hiyo kwa kutumia vigezo hivi, Mulokozi amezigawa tanzu na vipera vya Fasihi Simulizi kama ifuatavyo;
Masimulizi; hii ni tanzu ya Fasihi Simulizi yenye kusimulia habari fulani. Katika kugawa utanzu huu vigezo vilivyotumika ni pamoja na kigezo cha lugha ambapo lugha inayotumika katika masimulizi ni ya kinathari. Pia kigezo kingine ni kigezo cha muundo, mara nyingi masimulizi huwa na muundo unaojitofautisha na tanzu nyingine kama vile ushairi. Katika masimulizi muundo wake mara nyingi huwa wa moja kwa moja yaani mtiririko wa visa na matukio. Vilevile kigezo kingine ni kigezo cha wahusika ambapo katika kigezo hiki huhusisha wahusika wa pande mbili ambao ni mtendaji na watendwaji. Pia kigezo kingine ni kigezo cha namna ya uwasilishaji. Katika uwasilishwaji huwasilishwa na msimuliaji mbele ya hadhira. Kigezo kingine ni kigezo cha mandhari ambayo huwa maaluma kama vile chini ya mti mkubwa na uwanjani. Masimulizi pia hufanyika katika muda maalum. Mfano, baada ya kazi.
Masimulizi yamegawanyika katika tanzu kuu mbili ambazo ni tanzu za kihadithi (za kubuni) na tanzu za kisalua (kihisitoria). Tanzu za kihadithi zina kipera kimoja ambacho ni ngano. Ngano (vigano/hurafa), hizi ni hadithi za kimapokeo zitumiazo wahusika kama wanyama, miti na watu kuelezea na kuonya kuhusu maisha.  Vigezo vilivyotumika katika kugawa ngano ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya kinathari, kigezo cha dhima ambacho huelezea au kuonya kuhusu maisha na kufurahisha. Kigezo kingine kilichotumika ni kigezo cha wahusika ambao ni wanyama, miti na watu. Kipera hiki cha ngano kinajumuisha vijipera vifuatavyo ambavyo ni istiara, mbazi na kisa.
Istiara; hii ni hadithi ambayo maana yake ya wazi inawakilisha maana nyingine iliyofichika. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya mafumbo.
Mbazi; hii ni hadithi fupi yenye mafunzo itolewayo kama kielelezo wakati wa maongezi au kumkanya mtu. Kigezo kilichotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha dhima.
Kisa; hii ni hadithi fupi ya kufurahisha kuhusu tukio la kweli. Kigezo kilichotumika ni kigezo cha kidhima.
Utanzu mwingine wa masimulizi ni utanzu wa kisalua. Utanzu huu umegawanyika katika vipera vifuatavyo ambavyo ni visakale, mapisi, tarihi, kumbukumbu na visasili.
Visakale; haya ni masimulizi ya mapokeo juu ya wahenga au mashujaa wa kabila au taifa yenye kuchanganya chuku na historia (kama hadithi ya Liyongo). Vigezo vilivyuotumika hapa ni kigezo cha wahusika ambao wapo katika historia yaani mashujaa fulani. Kigezo kingine ni fani ya ubunifu.
Mapisi; haya ni maelezo ya kihistoria bila kutia mambo ya kubuni. Hapa pia kigezo kilichotumika ni kigezo cha dhima ambacho huelezea mambo ya kihistoria yaliyo ya kweli.
Tarihi; haya ni maelezo au jedwali la matukio muhimu na tarehe zake. Kigezo kilichotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambacho ni kuelezea matukio muhimu na tarehe zake. Pia kigezo kingine ni namna ya uwasilishaji ambapo huwasilishwa kwa kutumia jedwali na lugha yake huwa katika maandishi.
Kumbukumbu; haya ni maelezo ya matukio muhimu yanayomuhusu mtu binafsi au jamii ya watu. Hapa kimetumika kigezo cha fani, ambayo ni fani za wasifu na tawasifu. Pia kigezo kingine ni kigezo cha wahusika ambao ni watu.
Visasili; hiki ni kipera kinachofungamana na imani za dini na mizungu ya kajamii pia hizi ni hadithi za kale zenye kuwakilisha imani na mtazamo wa jamii inayohusika kuhusu asili ya ulimwengu na maisha yao. Kigezo kilichotumika ni kigezo cha kidhima ambacho huelezea shabaha ya maisha.
Utanzu mwingine wa Fasihi Simulizi ni utanzu wa Semi. Semi ni tungo au kauli fupi fupi za kisanaa zenye kubeba maana au mafunzo. Kigezo kilichotumika katika kugawa utanzu huu ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya mkato. Kigezo kingine ni kigezo cha kidhima ambacho ni kufunza.
Utanzu huu umegawanyika katika vipera vifuatavyo ambavyo ni methali, vitendawili, misimu, mafumbo na lakabu.
Methali ni semi fupi fupi zenye kueleza kwa mukhtasari fikra au mafunzo mazito yaliyotokana na uzoefu wa kijamii. Vigezo vilivyotumika katika kipera hiki ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya mafumbo. Vilevile kimetumika kigezo cha muundo ambapo methali huundwa na muundo wa pande mbili ambazo hutegemeana.
Vitendawili; huu ni usemi uliofumbwa ambao hutolewa kwa hadhira ili ufumbuliwe. Vigezo vilivyotumika ni kigezo cha lugha. Hapa lugha inayotumika ni lugha ya kimafumbo.
Misimu; ni semi za muda na mahali maalum ambazo huzuka na kutoweka kutegemea mazingira maalum. Hivyo vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha muktadha yaani hutokea wakati maalum na mazingira maalum.
Mafumbo; ni semi za maonyo au mawaidha ambazo maana zake za ndani zimefichika. Kigezo kilichotumika ni kigezo cha kidhima ambacho ni kuonya pamoja na kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya mafumbo.
Lakabu; haya ni majina ya kupanga ambayo baadhi ya watu hupewa au hujipatia kutokana na sifa zao za kimwili, kinasaba, kitabia au kimatendo. Kigezo kilicho tumika katika kipera hiki ni kigezo cha lugha ambayo lugha iliyotumika ni lugha kificho yaani maana yake hufichwa.
Utanzu mwingine wa Fasihi Simulizi ni ushairi. Huu ni utanzu wa fasihi simulizi unaowasilishwa kwa hadhira kwa njia ya uimbaji au ughani badala ya usemaji wa kawaida. Vigezo vilivyotumika katika kugawa utanzu huu ni kigezo cha lugha ambayo ni lugha ya kishairi. Pia kimetumika kigezo cha fani ambapo fani inayotumika ni wizani, lugha ya mkato, lugha ya mafumbo na uimbaji au ughani.
Katika utanzu huu kuna vipera viwili ambavyo ni nyimbo na maghani;
Nyimbo ni kila kinachoimbwa. Vigezo vilivyotumika katika kipera hiki cha ushairi ni kigezo cha fani ambapo huangalia muziki wa sauti ya muimbaji au waimbaji, muziki wa ala (kama ipo), matini au maneno yanayoimbwa. Pia kuna kigezo cha muktadha ambacho huzingatia hadhira inayoimbiwa na muktadha unaofungamana na wimbo huo, kwa mfano sherehe, ibada, kilio nakadhalika. Kwa vigezo hivi utanzu wa nyimbo umegawanyika katika vijipera vifuatavyo ambavyo ni, tumbuizo, bembea, kongozi, nyimbo za dini, wawe, tenzi, tendi, mbolezi, kimai, nyiso, nyimbo za vita, nyimbo za uwindaji, nyimbo za taifa, nyimbo za watoto na nyimbo za kazi.
Tumbuizo; hizi ni nyimbo za furaha ziimbwazo kuwafurahisha watu kwenye matukio mbalimbali kama vile ngomani au harusini. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambacho hulenga kuwafurahisha watu, pia kigezo kingine ni kigezo cha kimuktadha ambapo huwasilishwa katika matukio yanayoendana na dhima ya kufurahisha.
Bembea; hizi ni nyimbo za kubembeleza watoto. Kigezo kilichotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambapo hulenga kubembeleza watoto.
Kongozi; hizi ni nyimbo za kuaga mwaka. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuaga mwaka na kigezo cha kimuktadha ambapo muktadha wake ni muktadha maalum yaani huimbwa mwishoni mwa mwaka.
Nyimbo za dini; hizi ni nyimbo zinazoimbwa kwa lengo la kumsifu Mungu au miungu. Vigezo vilivyotumika ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kumsifu Mungu au miungu, pia kimetumika kigezo cha kimuktadha ambapo huimbwa katika muktadha wa kidini.
Wawe; hizi ni nyimbo za kilimo. Vigezo vilivyotumika ni kigezo cha kimuktadha ambapo huuimbwa wakati wa kulima, pia kigezo cha kidhima kimetumika ambapo dhima yake ni kuchapusha kazi.
Tenzi; hizi ni nyimbo ndefu za kimasimulizi au mawaidha. Kigezo kilichotumika ni kigezo cha kifani ambapo fani yake ni masimulizi au mawaidha.
Tendi; hizi ni nyimbo ndefu za masimulizi juu ya matendo ya mashujaa. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha kifani ambapo wahusika wa tendi ni watu wenye historia za matendo ya kishujaa, pia kigezo cha lugha kimetumika ambapo lugha yake ni ya kinathari.
Mbolezi; hizi ni nyimbo za kilio au maombolezo. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kimuktadha ambapo huwasilishwa katika muktadha wa maombolezo au kilioni/msibani, pia kimetumika kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuomboleza.
Kimai; hizi ni nyimbo zihusuzo shughuli za baharini. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuchapusha kazi. Vilevile katika kigezo cha kimuktadha kimai huwasilishwa katika mazingira ya baharini.
Nyiso; hizi ni nyimbo za jandoni. Vigezo vilivyotumika ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kutoa mafunzo kwa vijana kuhusu maisha ya utu uzima. Kigezo kingine ni kigezo cha kimuktadha ambapo nyiso huwasilishwa katika mazingira maalumu, kama vile porini nakadhalika.
Nyimbo za vita; hizi ni nyimbo ziimbwazo na askari wakati wa vita. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kimuktadha ambapo muktadha wake huwa ni wakati wa vita, na kigezo kingine ni kigezo cha wahusika au waimbaji ambapo waimbaji wake huwa ni maaskari.
Nyimbo za watoto, hizi ni nyimbo waimbazo watoto wakati wa michezo yao. Vigezo vilivyotumika ni pamoja na kigezo cha kimuktadha ambapo huwasilishwa wakati wa michezo ya watoto. Kigezo kingine ni kigezo cha wahusika au waimbaji ambapo waimbaji wake huwa ni watoto.
Nyimbo za uwindaji; hizi ni nyimbo ambazo huimbwa na makundi ya wawindaji wakati wa shughuli au sherehe zao. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha wahusika au waimbaji ambapo huimbwa na wawindaji na kigezo kingine ni kigezo cha kimuktadha ambapo huwasilishwa wakati wa shughuli au sherehe za uwindaji.
Nyimbo za Taifa; hizi ni nyimbo za kisifia Taifa au kabila. Kigezo kilichotumika hapa ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kusifia Taifa au kabila.
Nyimbo za kazi; hizi ni nyimbo zinazoimbwa katika shughuli mbalimbali kama vile, kulima, kutwanga, kusuka, uvuvi, uashi, useremala na kadhalika. Vigezo vilivyotumika hapa ni kigezo cha muktadha wa uwasilishaji ambapo huwasilishwa kulingana na shughali maalumu. Pia kigezo kingine ni kigezo cha kidhima ambapo dhima ya nyimbo za kazi ni kuchapusha kazi.                
Maghani; hiki ni kipera cha ushairi kinachotolewa kwa kalima badala ya kuimbwa. Kwa mujibu wa Wamitila (2003) maghani ni istilahi inayotumiwa kuelezea aina ya ushairi ambao hutolewa kwa kalima au maneno badala ya kuimbwa. Vigezo vilivyotumika katika kugawa utanzu huu ni lugha ambayo ni lugha ya kishairi. Pia ametumia kigezo cha wahusika ambapo wahusika wakuu ni binadamu. Hivyo vigezo hivi ndivyo vilivyopelekea utanzu huu kuwekwa kwenye utanzu wa ushairi.
Kipera hiki kina vijipera vitatu ambavyo ni maghani ya kawaida, sifo na maghani masimulizi. Maghani ya kawaida ni kundi ambalo tunaweza kuingiza fani mbalimbali za ushahiri simulizi kama vile ushairi wa mapenzi, siasa, maombolezo, kazi, dini ilimradi unaghanwa katika namna ya uwasilishwaji wake.
Sifo; hizi ni tungo za kusifu ambazo husifu watu, wanyama na mimea. Baadhi ya sifo huwa zinakashifu au kukejeli. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha wahusika, wahusika wake wakuu ni binadamu wanyama au mimea. Kigezo kingine ni muktadha ambao huelezea matukio yaliyopita au yaliyopo. Sifo huwa na tanzu muhimu kama vile vivugo (majigambo), pembezi na tondozi.
Kivugo; hili ni ghani la kujisifia, hutungwa na kughanwa na muhusika mwenyewe. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kijipera hiki cha sifo ni lugha, katika lugha zimetumika mbinu kama vile sitiari, mkato, vidokezo, ishara, takriri na vina. Kigezo kingine ni kigezo cha wahusika ambapo wahusika wake wakuu ni binadamu pia kimetumika kigezo cha muktadha ambapo muktadha wake hufungamana na tukio maalum katika maisha ya muhusika, mfano vitani. Vilevile katika kigezo cha uwasilishaji huweza kuwa na masimulizi ndani yake. Muundo wake hutegemea shabaha za mtunzi na jadi ya utunzi anayoiwakilisha hakiandikwi na kutungwa papo kwa papo.
Tondozi; hizi ni tungo za kusifu watu, wanyama au vitu. (Pembezi pia ni aina ya tondozi ambayo imekusudiwa watu wa aina fulani tu). Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha wahusika ambao ni wanyama na mimea. Mfano wa wanyama ni kama vile Simba. Kigezo kingine ni lugha ambayo ni lugha ya kishairi.  
Ghani masimulizi: hizi ni ghani ambazo hutambwa ili kusimulia hadithi, historia au tukio fulani. Vigezo vilivyotumika kugawa kipera hiki ni pamoja na kigezo cha lugha, lugha inayotumika katika kijipera hiki ni lugha ya kishairi na fani iliyotumika ni kusimulia hadithi/tukio kwa kirefu. Vile vile kuna kigezo cha namna ya uwasilishaji huambatana na ala za muziki mfano zeze na marimba.
Ghani masimulizi ina vipera vinne ambavyo ni rara, ngano, sifo na tendi.
Rara ni hadithi fupi nyepesi ya kishairi yenye visa vya kusisimua, vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni pamoja na lugha inayotumika, lugha inayotumika katika kipera hiki ni lugha ya kishairi, fani iliyotumika ni fani ya kihadithi ambayo ni hadithi fupi, nyepesi na inavisa vya kusisimua na kigezo kingine ni muktadha wa uwasilishaji ambapo huimbwa au kughanwa ikiambatana na ala za muziki.
Ngano; hizi ni hadithi za mapokeo zitumiazo wahusika kama wanyama, miti na watu katika kuelezea au kuonya kuhusu maisha. Katika kipera hiki kigezo kilichotumika ni muktadha wa uwasilishaji, kwamba huwasilishwa pamoja na ala ya muziki. Ngano huwa ghani masimulizi inapowasilishwa pamoja na ala ya muziki.
Sifo; hizi ni tungo za kusifu, kigezo kilichotumika ni muktadha wa uwasilishaji: sifo huwa ghani masimulizi inapoingiza muziki katika utondozi wake, lugha iliyotumika ni lugha ya kishairi.
Tendi; hizi ni ghani ndefu za masimulizi juu ya matendo ya mashujaa yenye uzito kijamii au kitaifa. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni fani ambayo ni huhusu matukio muhimu ya kihisitoria au ya kijamii. Kigezo kingine ni muktadha wa uwasilishaji, hutungwa na kuwasilishwa papo kwa papo.
Utanzu mwingine wa Fasihi Simulizi ni utanzu wa mazungumzo. Mazungumzo ni maongozi au maelezo ya mdomo katika lugha ya kawaida juu ya jambo lolote lile. Si kila mazungumzo ni fasihi ili mazungumzo yaitwe fasihi lazima yawe na usanii wa aina fulani. Vigezo vilivyotumika katika kugawa utanzu huu ni kigezo cha lugha ambapo lugha iliyotumika ni lugha ya kifasihi. Kigezo kingine ni kigezo cha kimuundo ambapo muundo wake huwa wa kidayalojia.
Utanzu huu wa mazungumzo una vipera vifuatavyo ambavyo ni hotuba, malumbano ya watani, soga, mawaidha na ulumbi.
Hotuba; haya ni mazungumzo ambayo huwasilishwa kwenye vikao rasmi vya kimila, kisiasa au kidini. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha lugha ambapo lugha yake huwa rasmi, sanifu na ya kisanaa. Kigezo kingine ni kigezo cha kimuktadha ambapo hotuba huwasilishwa katika mazingira maalumu kwa mfano katika vikao rasmi au mikutano.
Malumbano ya watani; haya ni mazungumzo yanayozingatia masharti yanayotawala uhusiano wao wa kiutani. Huweza kuwa utani wa kikabila, utani wa mababu au mabibi na wajukuu. Vigezo vilivyotumika katika ugawaji wa kipera hiki ni kigezo cha lugha ambapo lugha huwa ni ya kimafumbo. Kigezo kingine ni kigezo cha wahusika ambapo wahusika huwa na uhusiano wa karibu.
Soga; haya ni mazungumzo ya kupitisha wakati ili kusubiri kitu fulani. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kupitisha wakati. Kigezo kingine ni kigezo cha lugha ambapo lugha inayotumika siyo rasmi. Vilele kuna kigezo cha muktadha ambapo muktadha wake huwa ni mahali popote.
Mawaidha; haya ni maneno ya maonyo au mafunzo aghalabu huwa ya kidini na yenye muongozo. Kigezo kilichotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuonya au kutoa muongozo.
Ulumbi; huu ni uhodari wa kuzungumza ambao huwa ni wa kiufasaha na madoido. Vigezo vilivyotumika katika kugawa kipera hiki ni kigezo cha kifani ambapo lugha iliyotumika ni lugha ya kimadoido na kifasaha.
Utanzu mwingine katika Fasihi Simulizi ni utanzu wa maigizo. Maigizo ni michezo ambayo hutumia watendaji wa kuiga tabia na matendo ya watu au viumbe wengine ili kuburudisha na kutoa ujumbe fulani kwa hadhira. Vigezo vilivyotumika katika kutenga utanzu huu ni kigezo cha namna ya uwasilishaji ambapo huwasilishwa kwa kuiga matendo ya watu au wanyama. Kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kuburudisha, kuelimisha au kuonya. Pia kimetumika kigezo cha mandhari ambapo maigizo huambatana na matukio maalumu kama vile kwenye maadhimisho ya sherehe fulani na katika matukio ya kijamii.
Utanzu mwingine wa Fasihi Simulizi ni utanzu wa ngomezi. Ngomezi ni ile hali ya kupeleka ujumbe kwa kutumia mdundo wa ngoma. Vigezo vilivyotumika katika utanzu huu ni kigezo cha kifaa cha uwasilishaji ambacho ni ngoma. Pia kigezo kingine ni kigezo cha kidhima ambapo dhima yake ni kupeleka taarifa fulani kwa jamii. Mfano taarifa hiyo yaweza kuwa ya msiba, mkutano na kadhalika.
Pamoja na ugawaji huu wa tanzu na vipera vya Fasihi Simulizi uliofanywa na Mulokozi kwa kuzingatia vigezo vyake alivyovitumia, bado ugawaji huu unaudhaifu mkubwa tu. Udhaifu au changamoto za vigezo alivyovitumia Mulokozi ni kama ifuatavyo:-
Vigezo vyote hivi vinaweza kuingiliana; mfano kigezo cha kidhima, kama vile kuonya au kuelimisha huweza kuonekana katika tanzu zaidi ya moja au hata katika vipera mbalimbali.
Pia kigezo cha namna ya uwasilishaji huweza kuingiliana kutoka utanzu mmoja hadi mwingine. Mfano, katika utanzu wa masimulizi na mazungumzo.
Vilevile kigezo cha wahusika; kigezo hiki huweza kuingiliana katika utanzu mmoja na mwingine. Mfano, unaweza kuwa na hadithi yenye wanyama, binadamu, mizimu na kadhalika. Hivyo inakuwa si jambo rahisi kuona tofauti zilizopo.  
Kwa kuhitimisha, tunaweza kusema kwamba ni vigumu kuainisha tanzu na vipera vya Fasihi Simulizi kutokana na kwamba, Fasihi Simulizi hubadilika badilika kifani, kimaumbo na hata kimaudhui kwa kutegemea muktadha na namna ya uwasilishaji wake. Kwa mfano ngano iliyopo katika masimulizi ni tofauti na ngano iliyopo katika maghani. Hivyo basi tatizo hili linaweza kutatuliwa kwa kutumia istilahi tofauti katika vipera au tanzu zinazoingiliana.         
MAREJEO:
Mulokozi, M. M. (1989). Tanzu za Fasihi Simulizi: Katika Mulika 21. TUKI. Dar es Salaam.
Mulokozi, M.M. (1996). Utangulizi wa Fasihi Simulizi ya Kiswahili. TUKI. Dar es Salaam.
Wamitila, K.W. (2003). Kamusi ya Fasihi, Istilahi na Nadharia. Focus Publications Ltd.                                                       Nairobi.
TUKI, (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. (Toleo la Pili). East Africa: Oxford University Press na Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI).

KF 202 : FASIHI ANDISHI YA KISWAHILI

KF  202 :FASIHI ANDISHI YA KISWAHIlLI

UTANGULIZI:
Kadri jamii inavyobadilika ndivyo na historia inavyobadilika. Yote haya yanakwenda katika usambamba sawia. Hivyo kilichopo leo kinaweza kuwa sawa au tofauti na cha jana na ukweli wa jana waweza kuwa ukweli au uongo wa leo au kesho, kwa maana hiyo jamii na historia yake si tuli (static).
Vivyo hivyo hata katika fasihi ya Kiswahili hususani fasihi andishi. Jinsi jamii inavyobadilika kifikra, kiuchumi, kisiasa na kiutamaduni ndivyo na fasihi inavyobadilika. Kwa mantiki hiyo ni dhahiri kwamba, hata hadhi na nafasi ya fasihi andishi ya leo yaweza kuwa sawa au tofauti na fasihi andishi ya jana, juzi au kesho.
Hivyo basi, fasihi andishi ya Kiswahili tunaweza kuifananisha na kinyonga kutokana na tabia zake za kubadilika badilika kulingana na mazingira fawafu. Mabadiliko hayo huleta tija kubwa sana kwa taifa na jamii kwa ujumla.
===================================================================
Fasili mbalimbali:
Awali ya yote ni vyema kujua fasili ya dhana za msingi zilizojitokeza katika mada tajwa. Dhana hizo ni pamoja na fasihi ya Kiswahili na fasihi andishi. Kwa kuanza na fasili ya fasihi ya Kiswahili;
Kwa mujibu wa Mulokozi (1996) akiwanukuu Syambo na Mazrui (1992); fasihi ya Kiswahili ni ile iliyoandikwa kwa Kiswahili tu, iwapo inazungumzia utamaduni wa Kiswahili au utamaduni mwiningineo. Maadam fasihi hiyo imetumia lugha ya Kiswahili na imefuata mbinu za ufasaha wa lugha hiyo, basi kwa tafsiri yao ni fasihi ya Kiswahili.
Fasili hii ina mapungufu yafuatayo:
o   Kwanza wanadai kuwa, fasihi ya Kiswahili ni lile tu iliyoandikwa yaani fasihi andishi. Kitu ambacho si cha kweli, kwani ipo fasihi simulizi ya Kiswahili. Hivyo fasili yao inashindwa kufafanua uwepo wa fasihi simulizi ya Kiswahili. Fasihi ambayo ndiyo kongwe kabisa ukilinganisha na fasihi andishi.
o   Pili wanadai kuwa kazi yoyote ile ikiandikwa kwa Kiswahili basi ni fasihi ya Kiswahili hata kama ikaelezea utamaduni wa watu wengine.
Hivyo basi, kutokana na mapungufu hayo, tunaweza kusema kwamba; fasihi ya Kiswahili ni ile ambayo imeandikwa kwa lugha ya Kiswahili na inahusu au inaelezee utamaduni wa waswahili. Kwa mantiki hiyo, tunaweza kuhitimisha kuwa kuna fasihi ya Kiswahili na fasihi kwa Kiswahili.
Dhana ya pili ambayo nayo ni muhimu kufasili ni fasihi andishi ya Kiswahili. Hii tunaweza kuifasili kama ifuatavyo: Ni sanaa ya lugha iliyotungwa kwa lugha ya Kiswahili na kuwasilishwa kwa hadhira (wasomaji) kwa njia ya maandishi yenye kuelezea utamaduni na jadi wa waswahili.
Maana ya Hadhi na Nafasi ya fasihi andishi ya Kiswahili:
Hivyo basi, baada ya kuangalia fasili hizo sasa tuangalie kwa kina hadhi na nafasi ya fasihi ya Kiswahili kupitia mifano mbalimbali kutoka katika fasihi andishi ya Kiswahili.
Ili tuweze kujua hadhi ya fasihi ya Kiswahili ni vyema kwanza kujua nini maana ya hadhi. Hadhi katika maana ya kawaida ni ile hali inayomfanya mtu ajiheshimu na aheshimiwe; heshima.
Katika muktadha wa kifasihi tunaweza kusema kuwa, hadhi ya fasihi ya Kiswahili ni ile hali au namna ambavyo fasihi ya Kiswahili inavyochukuliwa/inavyoonekana. Je ina hadhi ya juu kati au chini?
Nadharia ya Msambao na hadhi ya fasihi andishi ya Kiswahili kitaifa na kiulimwengu:
Hivyo basi, tunapoizungumzia hadhi ya fasihi ya Kiswahili hususani fasihi andishi ya Kiswahili ni vyema kuhusianisha dhana hii na nadharia ya msambao “Diffusionism Theory”
 iliyoongozwa na mawazo ya ushawishi wa Grimms na Thompson.
Wanamsambao wanaamini kuwa, pale ambapo kazi mbili za fasihi toka jamii mbili tofauti zikifanana kimuundo au kimaudhui sababu ya ufanano huo ni kuwa, katika kipindi fulani hapo zamani, jamii hizo mbili ziliwahi kukutana kwa namna fulani na makutano baina ya jamii hizo yalisababisha hali ya kuazimiana kwa baadhi ya mila na desturi. Kwa hiyo uwepo wa fasihi andishi katika jamii ya waswahili  ulitokana na mwingiliano baina ya wageni na wenyeji.
Hiyo basi, uingiaji huu wa fasihi andishi katika jamii ya waswahili huonesha kuwa, hapo awali hakukuwa na fasihi andishi ya Kiswahili wala hadhi yake. Hadhi ya fasihi andishi ya Kiswahili imeanza kujitokeza baadaye na kujidhihirihsa kupitia nyanja mbalimbali kama vile elimu, utamaduni, jamii na hata siasa.
Kwa mantiki hiyo, tunaweza kuitazama hadhi ya fasihi andishi ya Kiswahili katika nyanja ya elimu kuanzia ngazi ya astashahada (cheti), stashahada, shahada, uzamili mpaka uzamifu.
Katika ngazi ya cheti yaani shule za msingi, sekondari na vyuo vya daraja la tatu fasihi andishi ya Kiswahili inahadhi kubwa sana. Kwa mfano, katika elimu ya msingi zipo kazi mbalimbali za fasihi andishi ya Kiswahili kama vile ushairi; mfano “Sizitaki Mbichi Hizi”, “Mama wa Kambo ni Mama”, “Karudi baba mmoja” na “Shairi la Moto na Maji”. Vilevile hata katika hadithi fupi kuna hadithi ya “Tola ala Gizani”, “Manenge na Mandawa”, “Nikiwa mkubwa” nk.
*    Kwa upande wa elimu ya sekondari, kidato cha kwanza mpaka cha sita kazi nyingi za fasihi andishi ya Kiswahili zinajidhihirisha kama ifuatavyo: kwa mfano; ushairi, (Mashairi ya Chekacheka, Wasakatonge, Kimbunga, Mapenzi Bora, Diwani ya Mloka, nk.), riwaya (Kiu ya Haki, Takadini, Vuta Nkuvute, nk.), tamthilia (Kwenye Ukingo wa Thim, Orodha, Ngoswe Penzi Kitovu cha Uzembe, Kivuli Kinaishi, Mfalme Juha, nk.)
*    Pia hata katika ngazi ya elimu ya juu bado kazi hizi za fasihi andishi ya Kiswahili zina hadhi kubwa na umuhimu mkubwa sana katika jamii ndio maana tunaona zinajitokeza kata huku. Kwa mfano; kuna kazi za ushairi kama vile Dhifa, Tenzi tatu za kale, Insha na Mashairi, nk.
*      Pia kuna riwaya kama vile: Moto wa Mianzi, Rosa Mistika, Nagona, Adili na Nduguze, Mzingile, Ufunguo Wenye Hazina nk.
*      Vilevile kuna tamthilia kama vile; Amezidi, Aliyeonja Pepo, Jogoo Kijijini na Ngao ya Jadi, Ngoma ya Ng’wanamalundi, Lina Ubani, Mkutano wa Pili wa Ndege, nk.
*   Licha ya hayo, pia tunaweza kuitazama hadhi ya fasihi andishi ya Kiswahili katika nyanja ya kijamii; fasihi andishi ya Kiswahili inahadhi kubwa sana. Hii ni kutokana na kazi mbalimbali zinazosomwa na jamii kupitia vitabu, majarida na hata magazeti. Kupitia kazi hizi hadithi mbalimbali zinasomwa na watu wanajipatia maarifa tofauti tofauti.
*     Vilevile hadhi ya fasihi inajibainisha hata katika utamaduni kupitia kazi mbalimbali, kwa mfano; fasihi andishi imepiga hatua kubwa sana katika kuenzi na kuendeleza utamaduni na historia ya makabila mbalimbali kitaifa. Mfano; zipo kazi za fasihi andishi ya Kiswahili kama vile vitabu ambavyo huelezea utamaduni pamoja na historia ya waswahili. Kwa mfano; Moto wa Mianzi (historia ya wahehe), Utenzi wa Nyakirukibi (historia ya wahaya) nk.
*     Licha ya fasihi ya Kiswahili kuwa na hadhi kubwa kitaifa kupitia nyanja hizo bado fasihi hii inaonesha juhudi za maendeleo yake na kuzidi kujipatia umaarufu katika shughuli mbalimbali kama ifuatavyo:
*  Katika kuhitimisha maadhimisho ya miaka 50 ya Chuo Kikuu cha DSM tarehe 25/10/2012 waandishi mbalimbali wa fasihi andishi ya Kiswahili walitunukiwa tuzo ya uandishi bora. Kwa mfano; Ibrahimu Hussein, S. Mohammed Ahamed, Luhumbika, Penina Muhando na E. Kezilahabi.
*      Vilevile katika kongamano la kimataifa la Kiswahili lililofanyika Blue Peal Hotel tarehe 04 hadi 06 /10/2012 waandishi mbalimbali walipata tuzo kutokana na kazi zao za uandishi. Pia robo tatu ya kazi zilizowasilishwa zilikuwa za fasihi andishi ya Kiswahili. Vilevile Balozi wa Kenya nchini Tanzania, alizindua kitabu chake alichokiandika kwa lugha ya Kiswahili kwenye Kongamano hilo.
*   Pia fasihi imepelekea kupanuka kwa idara ya Kiswahili ambapo kumekuwa na idara mbili ambazo ni Idara ya Lugha ya Kiswahili na Isimu pamoja na Idara ya Fasihi Mawasiliano na Uchapishaji. Maendeleo mazuri ya Idara ya Kiswahili yamechangiwa na wingi wa kazi za fasihi andishi, kwani robo tatu ya machapisho yote ni fasihi andishi.
v  Hadhi ya fasihi ya kiswahili kiulimwengu. Kwa kweli si jambo rahisi sana kusema kuwa fasihi ya Kiswahili hususani fasihi andishi ya Kiswahili inahadhi ya chini au juu. Ila kwa ujumla tunaweza kusema kwamba hadhi ya fasihi ya Kiswahili kiulimwengu haiko nyuma sana imepiga hatua kidogo japo si kwa kiasi kikubwa.  
*  Kwa mfano hadhi ya fasihi ya kiswahili kiulimwengu; fasihi andishi ya Kiswahili inafundishwa katika mataifa mbalimbali kama vile Korea, Afrika Kusini, Ujerumani, Marekani, Botswana, China, Italia nk.
*      Vilevile wanafunzi wa kigeni kutoka katika mataifa mbalimbali wanaokuja kwa lengo la kusoma lugha ya Kiswahili, wanasoma kazi mbalimbali za fasihi andishi ya Kiswahili kama vile hadithi fupi nk.
*    Pia zipo kazi mbalimbali za fasihi andishi ya Kiswahili zilizochapishwa nje ya nchi na bado zinaonekana kuwa na thamani sana. Mfano; baadhi ya kazi za mwandishi mashuhuri S. Robert.  
v  Nafasi ya fasihi ya Kiswahili kiulimwengu na kitaifa:
Nadharia ya sosholojia na nafasi ya fasihi andishi ya Kiswahili kitaifa na kiulimwengu
Katika kuangalia nafasi ya fasihi ya Kiswahili kitaifa na kiulimwengu tutazingatia nadharia ya wanasosholojia ambayo waasisi wake ni pamoja na Bronislaw Malinowski, A.R. Radcliffe- Brown na Franz Boaz. Wataalam hawa wanaweka mkazo zaidi katika utendaji na msisitizo juu ya dhima ya fasihi katika jamii. Nafasi ya fasihi andishi kitaifa na kiulimwengu ni kama ifuatavyo:
*      Kitaifa: fasihi ya Kiswahili kitaifa inanafasi kubwa sana, kwani dhima zake zina halisika katika jamii ya Tanzania na zinaendana na wakati uliopo. Miongoni mwa dhima hizo ni pamoja na kuelimisha, kuburudisha, kukuza uchumi nk.
*  Kiulimwengu: kupitia fasihi andishi ya Kiswahili tunao waandishi maarufu ambao ni kama chachu ya maendeleo ya Kiswahili nje na ndani ya jumuiya ya Afrika Mashariki kama vile E. Kezilahabi, F. Nkwera, J. Madumulla, I. Husseni, T.Sengo, Kingo, Chachage, Penina Mlama, S. Shaffi, Wamitila, E. Mbogo, Asha Kunemah, nk.
Waandishi hawa wametoa changamoto kubwa sana katika kukikuza na kukieneza Kiswahili pamoja na fasihi andishi ya Kiswahili.
Vilevile kupitia fasihi andishi ya Kiswahili wameonesha mafanikio makubwa katika kazi zao kiuchumi na hata katika ukombozi wa fikra za wanajamii.
Hitimisho:
Pamoja na kwamba, fasihi ya Kiswahili inahadhi na nafasi ya juu kitaifa bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali kama vile; watanzania wengi hawana utamaduni wa kusoma vitabu vya fasihi andishi ya Kiswahili, vilevile hata serikali haithamini sana mchango wa watunzi mbalimbali wa kazi za fasihi andishi na hii inatokana na kasumba kuwa lugha ya Kiswahili bado inahadhi ya chini hivyo, inapelekea hata kazi zake kutosomwa na watu wengi.
Marejeo:
BAKITA, (2004), Makala ya siku ya Kiswahili Kiswahili na Utandawazi, Dar es salaamu
Mulokozi, M. M. (1996) Utangulizi wa Fasihi ya Kiswahili. Dar es Salaam: Chuo Kikuu Huria.
TUKI, (2003) Makala za Semina ya Kimataifa ya Waandishi wa Kiswahili III: Fasihi Dar es Salaam.
TUKI, (2004) Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Dar es Salaam: TUKI.
Wamitila, K.W. (2003) Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi-Kenya: Focus                                            Publications Ltd.
Wamitila, K. W. (2004) Kichocheo cha Fasihi Simulizi na Andishi. Focus Publications Ltd.

KI 208 : FONOLOJIA YA KISWAHILI

KI  208 : FONOLOJIA   YA   KISWAHILI.

Fonolojia (hasa huitwa Sarufi Matamshi) ni tawi la sayansi ya isimu. Inashughulikia uchunguzi wa mfumo wa sauti katika lugha fulani, kwa mfano ugawanyaji wa irabu na konsonanti. Ala za sauti (vipashio vya utamkaji) zinatumika katika utamkaji wa fonimu (vitamkwa) za lugha husika. Mkondo wa hewa wakati wa utamkaji. Kuwepo na kutokuwepo kwa mguno wakati wa utamkaji (guna/siguna). Utanzu huu hushughulikia kanuni zinazotawala uchambuzi wa mfumo wa sauti, yaani, sauti kutamkwaje na wapi katika kinywa cha mwanadamu.
Matokeo ya uchunguzi wa kifonolojia yana umuhimu katika kubuni alfabeti. Dhana ya fonolojia inajipambanua vizuri zaidi ikifasiliwa kwa kutofautishwa na fonetiki. Wakati fonetiki ni taaluma inayochunguza sauti zitamkwazo na binadamu bila kuzihusisha na lugha yoyote, fonolojia huchunguza mfumo wa sauti wa lugha mahususi kama vile sauti za Kiswahili, Kiingereza, Kimwera, na Kinyaturu. ZINGATIA: Fonetiki huchunguza sauti zote zitamkwazo na binadamu; fonolojia huchunguza MFUMO WA SAUTI wa lugha mahususi.
Hivyo, fonetiki huchunguza sauti nyingi kadri iwezekanavyo, lakini fonolojia huchunguza sauti chache tu zilizomo katika mfumo wa sauti wa lugha husika. Mathalani, mfumo wa sauti wa lugha ya Kiswahili una sauti thelathini tu (irabu tano na konsonanti ishirini na tano).
Jambo lingine la kuzingatia ni vipashio vya kiuchambuzi vya matawi haya mawili. Wakati fonetiki kipashio chake cha msingi ni FONI, fonolojia kipashio chake cha msingi ni FONIMU. Kwa kuzingatia maelezo ya hapo awali, ni wazi kuwa FONI ni nyingi zaidi kuliko FONIMU, kwakuwa FONI ni kila sauti itamkwayo na binadamu, wakati FONIMU ni sauti zile tu zilizomo katika mfumo wa sauti wa lugha mahususi. Hivyo, kuna FONIMU za Kiswahili, za Kiingereza, za Kichina, n.k., lakini FONI si za lugha yoyote na wala uwezi sema kwa uhakika kuna FONI ngapi, kwakuwa bado kuna lugha nyingi duniani ambazo bado hazijatafitiwa.

Marejeo

  • TUKI 1990, "Kamusi Sanifu ya Isimu na Lugha", Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
  • Massamba, David 2004, "Kamusi ya Isimu na Falsafa ya Lugha", Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
Globe of letters.svg Makala hii kuhusu mambo ya lugha bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Fonolojia kama historia yake, uenezi au maendeleo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.

K I 208: FONOLOJIA YA KISWAHILI

KI 208 :FONOLOJIA YA KISWAHILI
UTANGULIZI
USULI WA TAALUMA YA FONOLOJIA
Neno fonolojia linatokana na maneno mawili ya Kigiriki phone-sauti za kusemwa na logos- taaluma/mtalaa. Masimulizi yanadai kuwa taaluma hii ilianza zamani sana kati ya mwaka
460 kabla ya Masihia huko India ya kale, ambapo mtu aliyeitwa Panini, na ambaye huaminika kuwa ni baba wa isimu aliandika kuhusu fonolojia ya Kisansikriti katika matini aliyoiita Shiva Sutras. Ni katika andiko hili ndipo alipobainisha kuwepo kwa dhana ambazo leo hii hujulikana kama fonimu, mofimu na mzizi.

Baada ya andiko hilo, habari za taaluma ya fonolojia ni kama zilipotea kabisa katika uwanja wa isimu hadi ilipofika karne ya 19 ambapo wanaisimu wengine waliibuka na kuzungumzia upya masuala ya fonolojia. Miongoni mwa wanaisimu wa mwanzo wanaotajwa kujihusisha na fonolojia ni Mpolandi "Jan Baudouin de Courtenay" , (pamoja na mwanafunzi wake wa zamani "Mikołaj Kruszewski" alipobuni neno fonimu mnamo mwaka 1876, na kazi yake, ijapokuwa hairejelewi sana, inachukuliwa kuwa ni mwanzo wa fonolojia mamboleo. Mwanaisimu huyu si tu alishughulikia nadharia ya fonimu, bali pia vighairi vya kifonetiki (ambavyo leo huitwa alofoni na mofofonolojia). Maandishi ya Panini (Sarufi ya Kisanskriti) pamoja na Jan Baudouin de Courtenay yalikuja kuwa na athari kubwa kwa anayeaminika kuwa baba wa nadharia ya Umuundo Mamboleo, Ferdinand de Saussure, ambaye pia alikuwa ni profesa wa Sansikriti.

Wanaisimu wote hawa walikuwa wanajaribu kulinganisha sauti za lugha za Asia Mashariki na za Ulaya, lengo lao likiwa ni kujua mizizi ya lugha zilizoitwa India-Ulaya. Kutokana na mkabala huo, katika kipindi hicho isimu ilikuwa Isimu-linganishi tu. Kutokana na tafiti zao hizo waliweza kupata maneno yenye sauti na maana zilizolingana, kufanana au kukaribiana. Utafiti huo uliweza kugundua jamii mbili za lugha ambazo ni jamii ya lugha za Kirumi na jamii ya lugha za Kijerumani. Baadhi ya wanaisimu mahususi kabisa wanaokumbukwa kuchangia katika maendeleo ya fonolojia ni pamoja na:
(i) Jan Baudouin de Courtenay (1845-1929)
Kama ilivyoelezwa hapo awali, huyu ni mwanaisimu aliyebuni dhana za foni na fonimu. Katika nadharia yake, alidai kuwa sauti za mwanadamu ni za aina mbili—foni na fonimu.  Alisema kuwa foni ni sauti za kutamkwa tu lakini fonimu ni sauti za lugha. Hata hivyo, de Courtenay hakutumia istilahi za foni na fonimu (kama zinavyotajwa sasa) bali alitumia istilahi za anthrophonics—foni na psychophonics—fonimu. Yeye alidai kuwa foni zipo karibu sana na taaluma ya kumuelewa binadamu pamoja na alasauti zake ambazo kwa hakika hutofautiana sana na za wanyama wengine. Na kuhusu fonimu, alidai kuwa zinahusu kumwelewa binadamu pamoja na akili zake na namna anavyofikiri katika akili yake. Alidai kuwa, mara nyingi, binadamu hupokea kinachotamkwa na kufasiliwa.
(ii) Ferdinand de Saussure (1887-1913)
Ni mwanaisimu wa Kiswisi anayejulikana kama baba wa isimu kutokana na mchango wake alioutoa katika taaluma hii. Yeye anakumbukwa zaidi kutokana na uwezo wake wa kutofautisha dhana alizoziita langue—mfumo wa lugha mahsusi na parole—matamshi ya mzungumzaji wa lugha husika. Langage hufafanuliwa kuwa ni uwezo alionao mzungumzaji wa lugha mahususi wa kuzungumza na kuelewa matamshi ya mzungumzaji mwingine wa lugha hiyohiyo. Ni sehemu ya lugha inayowakilisha maarifa kati ya sauti na alama. Ni mfumo wa alama kwa maana ya kiufundi tu. Dai lake la msingi ni kuwa alama inategemea vitu viwili—kitaja na kitajwa—hivyo ili mawasiliano yafanyike, mfumo wa ishara lazima ufahamike na ukubaliwe na wanajamii wote.
Kwa upande wa parole, anadai kuwa ni matendo uneni. Ni namna lugha inavyotamkwa katika hali halisi na mtu mmoja mmoja. Dhana ya parole inalingana na dhana ya performance (utendi) ya Noam Chomsky. Katika lugha, parole ni matamshi tofauti ya sauti moja—alofoni. Wanaisimu wanaonekana kukubaliana na madai ya Saussure kwakuwa inaelekea kuthibitika kuwa hakuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya kitaja na kitajwa [alama (lugha) na kinachowakilishwa (masilugha)], bali makubaliano baina ya wazungumzaji wa lugha moja husika ndiyo hutawala.
(iii) Nikolai Trubetzkoy (1890-1939)
Ni miongoni mwa waanzilishi wa taaluma ya fonolojia akichota mizizi ya taaluma ya isimu kutoka katika Skuli ya Prague. Mwanaisimu huyu aliandika misingi ya fonolojia kwa kutumia maarifa yaliyoibuliwa na Ferdinand de Saussure. Ni mtaalamu wa kwanza kufasili dhana ya fonimu. Aliandika vitabu vingi kwa lugha ya Kijerumani, miongoni mwake ni Grundzüge der Phonologie (Principles of Phonology, 1939), ambapo ni katika kitabu hicho ndimo alimotoa fasili ya fonimu pamoja na kubainisha tofauti baina ya fonetiki na fonolojia.
(iv) Noam Chomsky (1928-)
Huyu ni mwanaisimu wa Kimarekani anayevuma sana kwa mchango wake katika taaluma ya isimu kwa ujumla. Dhana za competence (umilisi) na perfomance (utendi) zimemfanya awe maarufu ulimwenguni. Dhana hizi zinaelezea tofauti baina ya maarifa na udhihirishaji wa maarifa hayo ya mtumiaji wa lugha. Katika fonolojia, Chomsky anakumbukwa kwa ufafanuzi wake wa dhana ya fonimu kwa mtazamo wa kisaikolojia. Anapochunguza dhana hii, hudai kuwa fonimu ni tukio la kisaikolojia, hivyo fonimu zimo kichwani mwa mzungumzaji wa lugha.
(v) Daniel Jones (1881-1967)
Ni mwanafonetiki kinara na maarufu kabisa katika nusu ya kwanza ya karne ya ishirini. Ni Mwingereza msomi ambaye alikuwa na shahada ya kwanza ya hisabati na shahada ya mahiri ya sheria, shahada ambazo hata hivyo, hakuwahi kuzitumia. Baadae, alisomea lugha na kuhitimu shahada ya uzamivu. Daniel Jones alifunzwa fonetiki na maprofesa mbalimbali, japokuwa aliathiriwa zaidi na Paul Passy na Henry Sweet. Hamu yake kuu ilikua kwenye nadharia ya fonetiki. Anafahamika zaidi kwa ufafanuzi wa dhana ya fonimu kwa mtazamo wa kifonetiki (ufafanuzi wake tutauchunguza katika sehemu ya mitazamo ya dhana ya fonimu).      
FONETIKI NA FONOLOJIA
Fasili ya taaluma ya fonolojia haiwezi kukamilika, na pengine kueleweka, iwapo hakuna linalosemwa kuhusiana na taaluma ya fonetiki. Hali hii inatokana na ukweli kuwa kuna uhusiano wa kinasaba kati ya fonolojia na fonetiki. Massamba na wenzake (2004:5) wananeneleza ukweli huu kwamba:
…fonetiki na fonolojia ni matawi mawili tofauti ya isimu lakini yenye kuhusiana sana. Uhusiano wa matawi haya unatokana na ukweli kwamba yote mawili yanajihusisha na uchunguzi na uchambuzi unaohusu sauti za lugha za binadamu.
Kutokana na ukweli huu, jitihada za kufasili dhana ya fonolojia inaelekea kuwa nyepesi, dhana hizi mbili zinapofasiliwa kwa mlinganyo. Tuanze na fonetiki:
FONETIKI NI NINI?
Fonetiki ni tawi la isimu linalochunguza sauti za kutamkwa na binadamu ambazo huweza kutumika katika lugha asilia. Massamba na wenzake (kama hapo juu) wanafasili fonetiki kuwa ni tawi la isimu linalohusika na uchunguzi na uchambuzi wa taratibu za utoaji, utamkaji, usafirishaji, usikiaji, na ufasili wa sauti za lugha za binadamu kwa ujumla. Wanasisitiza kwamba, kinachochunguzwa katika fonetiki ni [maumbo] mbalimbali ya sauti zinazoweza kutolewa na alasuti za binadamu (yaani sauti za binadamu zinazotamkwa tu). Kipashio cha msingi cha uchambuzi wa kifonetiki ni foni.
Foni ni sauti yoyote inayotamkwa na binadamu na inayoweza kutumika katika lugha fulani. Hivyo basi, foni ni nyingi sana na hazina maana yoyote. Wanafonetiki hudai kuwa foni zimo katika bohari la sauti (dhana dhahania) ambalo kila lugha huchota sauti chache tu ambazo hutumika katika lugha mahususi. Sauti chache zinazoteuliwa na lugha mahususi kutoka katika bohari la sauti huitwa fonimu.
Matawi ya Fonetiki: Kuna mitazamo miwili tofauti kuhusiana na matawi ya fonetiki. Mtazamo wa kwanza ni unaodai kuwepo matawi matatu; na mtazamo wa pili ni unaodai kuwepo matawi manne. Mtazamo wa kuwepo matawi matatu unataja fonetiki matamshi, fonetiki akustika, na fonetiki masikizi. Mtazamo wa kuwepo matawi manne (kama Massamba na wenzake (kama hapo juu), pamoja na matawi tuliyokwisha yataja, wanongezea tawi fonetiki tibamatamshi.
Fonetiki matamshi huchunguza jinsi sauti za lugha zinavyotamkwa kwa kutumia alasauti. Hususani, huchunguza namna na mahali pa kutamkia sauti husika. Fonetiki akustika huchunguza jinsi mawimbi ya sauti yanavyosafiri kutoka katika kinywa cha mtamkaji hadi kufika katika sikio la msikilizaji. Fonetiki masikizi hujihusisha na mchakato wa ufasili wa sauti za lugha, hususani uhusiano uliopo baina ya neva za sikio na za ubongo. Na fonetiki tibamatamshi ni tawi jipya lililozuka mwanzoni mwa karne hii, ambalo huchunguza matatizo ya utamkaji ambayo binadamu huweza kuzaliwa nayo au kuyapata baada ya kuzaliwa. Ni tawi linalojaribu kutumia mbinu za kitabibu kuchunguza matatizo na kutafuta namna ya kuyatatua.
FONOLOJIA NI NINI?
Fonolojia ni taaluma ya isimu inayochunguza mifumo ya sauti za kutamkwa zinazotumika katika lugha asilia mahususi za binadamu. Inapolinganishwa na fonetiki, inasisitizwa kuwa fonolojia ni tawi la isimu linalochunguza mifumo ya sauti za lugha mahususi tu, kama vile sauti za Kiswahili, Kiingereza, Kigogo, n.k. Hata hivyo, wapo wanaisimu wanaoelekea kukubaliana kuwa kuna fonetiki ya lugha mahususi pia, na kuna fonolojia ya jumla, na fonetiki ya lugha mahususi. Mathalani, Massamba (1996) licha ya kufasili fonolojia kuwa ni taaluma ya isimu inayochunguza mfumo wa sauti za lugha mahususi, anaenda mbele zaidi na kudai kuwa fonolojia inaweza kuchunguza sauti kwa ujumla wake bila kuzihusisha na lugha mahususi.
Akmajian na wenzake (2001), nao wanadokeza msimamo kama wa Massamba wanapodai kwamba fonolojia inaweza kuchunguzwa kwa mitazamo miwili tofauti. Kwanza, fonolojia kama tawi dogo la isimu linalochunguza mfumo na ruwaza za sauti za lugha mahususi ya binadamu; na pili, fonolojia kama sehemu ya nadharia ya jumla ya lugha ya binadamu inayohusika na tabia za jumla za mfumo wa sauti za lugha asilia za binadamu. Katika mhadhara huu, hata hivyo, tutakuwa wafuasi wa mtazamo unaoona kuwa fonolojia ni tawi la isimu linaloshughulikia mfumo wa sauti za lugha mahususi, hivyo tuna, kwa mfano, fonolojia ya Kiswahili, fonolojia ya Kiingereza, fonolojia ya Kiha, fonolojia ya Kihehe, na fonolojia ya Kibena. Kipashio cha msingi cha fonolojia ni fonimu.
FONIMU
Ni kipashio kidogo kabisa cha kifonolojia kinachoweza kubadili maana ya neno. Hivyo basi, fonimu ina maana, kwakuwa inaweza kubadili maana ya neno inapobadilishwa nafasi katika neno husika. Foni chache zilizoteuliwa kutoka katika bohari la sauti ili zitumike kwenye mfumo wa sauti za lugha mahususi ndiyo fonimu. Hivyo, fonimu ni chache ikilinganishwa na foni. Idadi ya fonimu za lugha hutofautiana kati ya lugha moja na nyingine. Mathalani, Kiarabu kina fonimu ishirini na nane (28), Kiswahili kina fonimu thelathini (30), Kifaransa kina fonimu thelathini na tatu (33), na Kiingereza kina fonimu arobaini na nne (44). Sauti ambayo huweza kubadilishwa nafasi yake katika neno lakini maana ikabaki ileile huitwa alofoni.
Alofoni ni kipashio cha kifonolojia kinachotaja hali ambapo fonimu moja hutamkwa na kuandikwa tofautitofauti bila kubadili maana ya neno. Mfano:
Fedha na feza

Sasa na thatha
Heri na kheri
Kwa kifupi, alofoni ni matamshi tofautitofauti ya fonimu (sauti) moja.
MITAZAMO YA DHANA YA FONIMU
Juhudi za kufasili dhana ya fonimu zilizofanywa na wanaisimu mbalimbali zimezua mitazamo mbalimbali ya namna ya kuchambua dhana hii. Hadi sasa, mitazamo mitatu ifuatayo ndiyo hujulikana zaidi.
Fonimu ni Tukio la Kisaikolojia
Huu ni mtazamo uliokuzwa na kutetewa na wanasarufi geuzi-zalishi, mwanzilishi wake akiwa ni Noam Chomksy. Kwa mujibu wa mtazamo huu, fonimu ni dhana iliyo katika akili ya mzungumzaji wa lugha. Mtazamo huu unadai kuwa kila mzungumzaji wa lugha ana maarifa bubu ya idadi na jinsi ya kutamka fonimu za lugha yake. Chomsky anayaita maarifa haya kuwa ni umilisi (competence). Anadai kuwa maarifa haya ya fonimu hufanana kwa kiasi kikubwa miongoni mwa wazungumzaji wa lugha moja husika. Kinachotofautiana ni jinsi ya kudhihirisha (kutamka)  fonimu hizo, yaani utendi (perfomance). Chomsky anabainisha kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kuhitilafiana baina ya umilisi na utendi kutokana na matatizo mbalimbali ambayo mzungumzaji hukabiliana nayo. Matatizo hayo ni kama vile uchovu, ulemavu wa viungo vya matamshi (alasauti za lugha), athari za mazingira, ulevi, na maradhi. Hivyo, kutokana na hali hii, fonimu hubaki kuwa tukio la kiakili, yaani kisaikolojia tu.